Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kigogo Bakwata akatwa mkono, mtuhumiwa auawa

PANGA Ed Kigogo Bakwata akatwa mkono, mtuhumiwa auawa

Wed, 7 Feb 2024 Chanzo: MwanahalisiOnline

Katibu wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), Wilaya ya Bukoba Mjini, Hamza Zacharia Abdallah, amenusurika kifo baada ya kucharangwa mapanga yaliyomsababishia kupoteza kiganja cha mkono wa kushoto.

Zacharia anadaiwa kutendewa ukatili huo na Abdulbarik Yahaya, aliyekuwa mtunza vifaa vya mradi wa ujenzi wa jengo la baraza hilo (BAKWATA Complex), wilayani Bukoba Mjini, baada ya Katibu huyo kumtuhumu kwa ubadhirifu. 

Akizungumza nasi kwa njia ya simu, leo tarehe 6 Februari 2024, Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Blasius Chatanda, amesema tukio hilo limetokea wiki iliyopita, baada ya Yahaya kumvamia Seikh Hamza ofisini kwake majira ya asubuhi na kuanza kumcharanga mapanga.

Amesema, baada ya mtuhumiwa huyo kuanza kumcharanga mapanga hadi kiganja cha mkono wake wa kushoto kukatika, majirani waliingilia kati kwa ajili ya kumdhibiti lakini alikaidi kitendo kilichowapeleka waanze kumshambulia na kumsababishia majeraha ambapo alifariki wakati akiwa njiani akikimbizwa hospitalini kwa ajili ya matibabu.

Kamanda Chatanda amesema chanzo cha tukio hilo ni Sheikh Hamza kumtuhumu mlinzi huyo kwa ubadhirifu wa fedha katika ujenzi wa jengo hilo. Ameongeza kuwa mhanga wa tukio hilo anauguza majeraha katika Hospitali ya Rufaa ya Bukoba.

“Mtuhumiwa alikuwa stoo keeper wa mradi wa BAKWATA Complex, jina lake nimelisahau sababu kwa harakaharaka sina taarifa. Yule bwana alikuwa ameondolewa kwa sababu ya kutuhumiwa sio muadilifu hivyo baada ya kuondolewa akamtuhumu Hamza kuwa yeye ndiyo sababu ya kumfanya atoke kwenye ile nafasi. Tukio hilo lilitokea nadhani kati ya tarehe 1 au 2 Februari mwaka huu,” amesema Kamanda Chatanda na kuongeza:

“Kesho yake baada ya kuondolewa saa 5.00 asubuhi pale alipokuwa anakaa yule mzee alikuwa anashona akamfuata akaanza kumcharanga mapanga mkono ukaachia, lakini majirani walioona kitendo kile wakaingia kuamulia na yeye hakukubali bahati mbaya nao wakampiga wakamjeruhi Askari wakaingilia kati wakampeleka hospitali lakini njiani akafariki.”

Chanzo: MwanahalisiOnline