Dar es Salaam. Kesi inayowakabili Vigogo 18 wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRC) imeshindwa kuendelea na ushahidi kutokana na Wakili wa Serikali anayeendesha shauri hilo kupata udhuru.
Pia vigogo hao wanakabiliwa na mashtaka 15 ya matumizi mabaya ya madaraka, ikiwemo kuidhinisha michoro 274 ya mabehewa ya mizigo kwa Kampuni ya Hindusthan kinyume na mkataba wa zabuni.
Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Nickson Shayo aliieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa shauri hilo lilikuja kwa ajili kusikilizwa ushahidi lakini wakili wa Takukuru, Maghela Ndimbo amepata udhuru.
Baada ya maelezo hayo Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo Kelvin Mhina aliahirisha shauri hilo hadi kesho litakapokuja kwa ajili kusikilizwa ushahidi.
Washtakiwa katika kesi hiyo ni Mkurugenzi Mkuu wa TRL, Kipallo Kisamfu, Gilbert Minja, Pascal Mafikiri, Mathias Massage, Anthony Munishi, Charles Ndenge, Ferdinand Soka, Muungano Kaukunda, Joseph Mlinda, Kedmond Mapunda, Lowland Simtengu, Ngoso Mwakilembe, Yonah Shida, Malumbo Malumbo, Stephen Kavombwe, Donatus Bandebe, John Charles na Ally Mwangila.
Katika shtaka la kwanza dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa TRL, Kipallo Kisamfu inadaiwa Machi 21 mwaka 2013 huko katika makao makuu ya kampuni hiyo, alitumia madaraka yake vibaya kwa kusaini mkataba wa zabuni kwa Kampuni ya Hindusthan Engeering and Industries Limited bila kuhakiki mkataba huo utatekelezeka kwa kuzingatia masharti ya mkataba.
Habari zinazohusiana na hii
- Tanzania katika ushiriki wa mtandao wa usambazaji umeme SADC
- Mkongo wa Taifa Tanzania kupenya nchi za SADC