Dar es Salaam. Upande wa mashtaka katika kesi ya kutoa maneno ya uchochezi inayomkabili Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu umesema wanamsubiri mbunge huyo ili kuendelea na kesi hiyo.
Wakili wa Serikali, Janeth Magoha amedai leo Jumanne Machi 5, 2019 mbele ya Hakimu Mkazi, Salum Ally kuwa kesi hiyo imekuja kwaajili ya kuendelea lakini mshtakiwa huyo yuko nje ya nchi kwenye matibabu hivyo wanaomba tarehe nyingine ya kutajwa.
“Kesi imekuja kwaajili ya kuendelea lakini mshtakiwa yupo nje ya nchi kwaajili ya matibabu tunaomba tarehe nyingine ya kutajwa ili kuangalia kama mshtakiwa atakuwa amerejea ili kesi iweze kuendelea,” amesema wakili Magoha
Lissu ambaye yuko nchini Ubeljiji kwaajili ya matibabu alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Juni 30, 2016 na kufunguliwa kesi ya uchochezi Na.233/2016.
Katika Kesi hiyo upande wa mashtaka una jumla ya mashahidi 15 ambapo tayari shahidi mmoja ameshatoa ushahidi mahakamani hapo.
Katika kesi hiyo, Lissu anakabiliwa na kesi ya uchochezi akidaiwa Juni 28, 2016, akiwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, alitoa kauli za uchochezi kuwa:
“Mamlaka ya Serikali mbovu ni ya kidikteta uchwara inahitaji kupingwa na kila Mtanzania kwa nguvu zote. Huyu dikteta uchwara lazima apingwe kila sehemu.
“Kama uongozi utafanywa na utawala wa kijinga, nchi inaingia ndani ya giza nene.’’
Soma Zaidi: Kesi ya Lissu kuendelea Februari