Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kesi ya anayedaiwa kughushi saini ya mkewe kusikilizwa mwezi ujao

Kesi Pic Uda Kesi ya anayedaiwa kughushi saini ya mkewe kusikilizwa mwezi ujao

Mon, 13 Feb 2023 Chanzo: Mwananchi

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imepanga Machi 2, 2023 kuanza kusikiliza kesi ya kughushi saini ya mkewe na kujipatia Sh 140 milioni inayomkabili mfanyabiashara Seleman Maziku.

Maziku, mkazi Kitunda wilaya ya Ilala, anadaiwa kujipatia kiasi hicho cha mkopo kutoka benki ya Stanbic baada ya kuwasilisha nyaraka ya kughushi ikionyesha kuwa mke wake aitwaye Schola Bundala ametoa ridhaa kwa mume wake kuchukua mkopo huo katika benki hiyo.

Leo Februaria 13, 2023, kesi hiyo ya jinai namba 200/2022 ilipangwa kwa ajili ya upande wa mashtaka kuanza kusikiliza ushahidi lakini hakimu anayesikiliza shauri hilo ana majukumu mengine ya kiofisi.

Wakili wa Serikali, Adolf Verandumi ameieleza Mahakama hiyo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Richard Kabate wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili ya ushahidi.

Hakimu Kabate baada ya kusikiliza maeneo hayo, ameahirisha kesi hiyo hadi Machi 2, 2023 kwa ajili kusikilizwa na mshtakiwa yupo nje kwa dhamana.

Inadaiwa kuwa Desemba 10, 2022 katika eneo lisilojulikana jijini Dar es Salaam, mshtakiwa bila ya ridhaa kutoka kwa mke wake alisaini nyaraka za mkopo akionyesha kuwa imesainiwa na Schola.

Maziku baada ya kusaini nyaraka hiyo, aliiwasilisha benki ya Stanbic kama moja ya taratibu za kibenki zinavyotaka, kitendo kilichosababisha mshtakiwa alijipatia mkopo wa Sh140 milioni uliotolewa na benki hiyo wakati akijua kuwa nyaraka hiyo ameghushi na haijaridhiwa na mke wake.

Desemba 18, 2022 Schola aligundua kuwa mume wake ameghushi saini yake na kwenda kutoa taarifa kituo cha polisi na baadaye Maziku alikamatwa kwa ajili ya kuhojiwa.

Mshtakiwa baada ya kukamatwa alichukuliwa sampuli za maandishi ikiwemo saini yake aliyoiweka na kushuhudiwa na wakili wake, Castor Rwekiza pamoja na saini ya Schola na kisha kupelekwa katika maabara kwa ajili ya uchunguzi.

Hata hivyo, uchunguzi ulibaini kuwa saini iliyowekwa katika nyaraka hizo iliwekwa na mshtakiwa na sio mke wake.

Baada ya kukamalika uchunguzi wa awali, mshitakiwa alifikishwa Mahakamani hapo kujibu tuhuma zinazomkabili.

Chanzo: Mwananchi