Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kesi ya aliyechoma kwa magunia ya mkaa yarudishwa Kisutu

MAUAJI MKEWE Kesi ya aliyemuua mkewe na kumchoma kwa magunia ya mkaa yarudishwa Kisutu

Wed, 31 May 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Jalada la kesi la mauji inayomkabili mfanyabiashara Khamis Luwonga (38) anayetuhumiwa kumuua mkewe Naomi Marijani na kumchoma moto kwa kutumia magunia mawili ya mkaa, limerudishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwa ajili ya usikilizwaji wa uamuzi kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Mshitakiwa kupitia mawakili wake, Mohamed Majaliwa, Fatuma Abdul na Zidadi Mikidadi aliwasilisha mahakamani hapo maombi ya kutaka kupata maelezo ya uhalali wa kesi ya mauji namba 5, 2022 iliyopo Mahakama ya Kisutu na kumuachia huru mshitakiwa.

Katika uamuzi wa maombi hayo, Jaji Obadia Bwegoge ambaye ndiye aliyeshikiliza maombi hayo alisema kulingana na sheria inavyotaka mahakama hiyo haina mamlaka ya kufanya uamuzi wa kumuachia huru mshitakiwa.

Aidha, alielekeza jalada la kesi hiyo lirudishwe Mahakama ya Kisutu, ili hakimu anayeisikiliza shauri hilo atolee uamuzi juu ya uhalali wa kuwepo kwa kesi hiyo ya mauaji katika mahakama hiyo.

Jalada hiyo limesharudishwa mahakamani hapo na kupangiwa tarehe, Juni 8, 2023 mshitakiwa atafikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Ramadhani Rugemalila kwa ajili kusikilizwa kwa uamuzi wa Mahakama Kuu.

Jaji Bwegoge alisema ametoa uamuzi huo kwa kuangalia majibu ya maswali mawili, kama maombi yaliyoletwa ni kweli sheria imevunjwa? na la pili ni kama Mahakama Kuu ina mamlaka ya kutoa uamuzi juu ya maombi hayo.

Alisema kwa kujibu swali la kwanza juu ya uhalali wa maombi hayo kisheria, sheria ipo wazi imeelekeza ni namna gani upande wa mashitaka unaweza kuamua kama hautakuwa na nia ya kuendele na shuari.

"Sheria imesema kwamba upande wa mashitaka unaweza kuiandikia mahakama au kuiambia kwa mdomo kama haina nia ya kuendelea na shauri na mshitakiwa anatakiwa aachiwe huru kama yupo gerezani," alisema.

Pia alisema kama upande wa mashitaka utamkamata tena mshitakiwa kwa kosa lile lile baada ya kuachiliwa inatakiwa ushahidi ukamilike na siku ya kwanza anapoletwa mahakamani kesi isikilizwe.

"Lakini katika maombi haya mshitakiwa alikamatwa kwa kosa lile lile na ameshapandishwa mahakamani zaidi ya mara tano kwa kesi ya kutajwa," alisema.

"Hii inajidhihirisha katika rekodi zilizopo katika jalada la kesi ya inayoendelea Mahakama ya Kisutu. Hivyo basi upande wa mashitaka ni dhahiri umekeuka sheria," alisema Jaji Bwegoge

Alisema katika swali la pili, kulingana na sheria Mahakama Kuu haina mamlaka ya kufanya uamuzi ya kumuachilia mleta maombi, ambapo mshitakiwa aliomba hivyo kwa madai kuwa upande wa mashitaka hauna ushahidi wa kutosha wa kumshitaki.

"Kulingana na sheria ilitaka maombi haya yaombwe mbele ya mahakama iliyokuwa inaendesha kesi hiyo, naelekeza jalada lirudishwe Mahakama ya Kisutu na mheshimiwa anaesimamia kesi ya mleta maombi alitolee uamuzi juu ya uhalali wake," alisema.

Katika kesi hiyo ya muaji namba nne ya mwaka 2019, mshitakiwa Luwonga ambaye ni Mkazi wa Kigamboni, Dar es Salaam anadaiwa Mei 15, 2019 akiwa Gezaulole eneo la Kigamboni alimuua Naomi Marijani.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live