Dar es salaam. Kesi ya kutoa lugha chafu dhidi ya Rais wa Tanzania John Magufuli inayomkabili Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee imeshindwa kuendelea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutokana na kuwa mgonjwa.
Wakili wa Serikali, Silvia Mitanto amedai leo Jumanne Juni 11,2019 mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya kusikilizwa lakini mshtakiwa ni mgonjwa na mdhamini wake yupo.
Hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo hadi Julai 9 mwaka 2019 kwa ajili ya kuendelea na usikilizaji.
Mpaka sasa mashahidi watatu wa upande wa mashitaka wameshatoa ushahidi katika kesi hiyo akiwamo Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Urafiki, Mrakibu wa Polisi (SP) Batseba Kasanga.
Katika kesi ya msingi inadaiwa Julai 3, 2017 katika ofisi za makao makuu ya Chadema zilizopo mtaa wa Ufipa wilayani Kinondoni, Mdee alitamka maneno dhidi ya Rais John Magufuli kuwa, ‘anaongea hovyo, anatakiwa afungwe breki,’ kitendo kinachodaiwa kuwa ni kumdhalilisha Rais na kusababisha uvunjifu wa amani.
Pia Soma
- Dk Sebahene adai rushwa Tanzania bado tatizo
- Mwanafunzi apigwa risasi akiingia Ikulu Kenya
- Kisena, mkewe waendelea kusota rumande
- Serikali ya Tanzania yaomba hukumu ya Sheikh Ponda kutenguliwa