Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kesi viongozi CCM kuomba rushwa kuanza kusikilizwa Julai 22

65573 Ccm+pic

Fri, 5 Jul 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Mahakama ya Wilaya ya Ilala Julai 22 ,2019 itaanza kusikiliza kesi ya kuomba rushwa inayowakabili viongozi watatu wa CCM.

Viongozi hao wanadaiwa kuomba rushwa ya Sh5 milioni na kupokea Sh3 milioni.

Watuhumiwa ni Katibu wa CCM tawi la Amana, Jenifer  Mushi (47); Katibu Kata Ilala, Devotha Batulake (43) na Katibu Uhamasishaji Mkoa wa Dar es Salaam, Frank Mang'ati (38).

Uamuzi huo wa mahakama umekuja baada ya wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Veronica Chimwada  kueleza kuwa wanatarajia kuwaita mashahidi saba wa upande wa mashtaka kutoa ushahidi kwenye kesi hiyo na vielelezo visivyopungua vinne.

Hatua hiyo imekuja baada ya upande wa mashtaka kukamilisha  upelelezi na washtakiwa hao kusomewa maelezo ya awali mbele ya hakimu mfawidhi,  Martha Mpaze.

Wakisomewa maelezo hayo ya awali washtakiwa wote walikubali maelezo yao binafsi ikiwamo shughuli wanazozifanya  ndani ya CCM.

Pia Soma

Mshtakiwa wa kwanza, Jenifer Mushi alikubali  kusaini fomu ya mtego ya Takukuru na mshtakiwa wa tatu, Frank alikubali kuwa utaratibu wa upangishaji ni lazima waombaji kuandika barua na wote waliyakana mashtaka yote yanayowakabili.

Katika kesi hiyo ya jinai namba 250 ya mwaka 2019 washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuwa  Machi 21,2019 katika klabu ya wazee Amana walishawishi rushwa ya Sh5 milioni kutoka kwa mmiliki wa kampuni ya Daluni  East Africa Transport, Daud Kalaghe ili waweze kumpatia kiwanja namba 41 Y kinachomilikiwa na CCM kwa shughuli ya biashara.

Inadaiwa kuwa Machi 22, 2019 katika eneo la Msimbazi Sekondari washtakiwa hao walijipatia rushwa ya Sh3 milioni kutoka kwa Kalaghe ili waweze kumpatia kiwanja namba 41 Y kinachomilikiwa na CCM kwa shughuli ya biashara.

Washtakiwa  hao wapo nje kwa dhamana baada ya kukamilisha  masharti ya kila mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili.

Washtakiwa hao walikamatwa Machi 21, 2019 baada ya kuwekewa mtego na Takukuru.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz