Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeutaka upande wa mashtaka kufuatilia upelelezi umefikia wapi katika kesi ya mauaji inayomkabili askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania ( JWTZ), Ramadhani Mlaku.
Hatua hiyo imekuja baada ya Wakili wa Serikali, Tully Helela kudai kuwa shauri hilo limekuja kwa ajili ya kutajwa na upelelezi bado haujakamilika.
Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba amesema upande wa mashtaka wafuatilie huo upelelezi umefikia wapi kwa kuwa kesi hiyo ni ya muda mrefu.
Hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo hadi Mei 13,2019 itakapotajwa tena, na mshtakiwa amerudishwa rumande kutokana na shtaka linalomkabili kutokuwa na dhamana.
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, Mlaku anadaiwa kutenda kosa hilo Oktoba 30, 2017, eneo la Upanga, makao makuu ya jeshi hilo.
Mlaku ambaye ni askari wa kambi ya jeshi hilo iliyopo Makongo, anadaiwa kumuua mwanajeshi wenzake mwenye namba MT 79512, Sajenti Saimon Munyama.