Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kesi mauaji ya Dk Mvungi yapata hakimu mwingine

63336 Pic+mvungi

Wed, 19 Jun 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar Es Salaam. Hatimaye washtakiwa  sita kwenye kesi ya mauaji ya aliyekuwa Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Dk Sengondo Mvungi wamepewa Hakimu mwingine.

Hatua hiyo imetokana na washtakiwa hao kumkataa Hakimu wa awali, ambaye ni Hakimu Mwandamizi wa mahakaka hiyo, Augustina Mmbando  aliyekuwa anaendesha kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Kwa sasa kesi hiyo  yenye namba  6/2018 itasikilizwa, mbele ya Hakimu Mwandamizi, Augustine Rwizile wa Mahakama ya Kisutu.

Washtakiwa ni pamoja na Msigwa Matonya (35), Mianda  Mlewa(45), Paulo Mdonondo (35), Longishu Losindo (34), Juma Kangungu (34) na John Mayunga (60), walipanda kizimbani jana Jumanne Juni 18,2019 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya Hakimu Mkazi Augustine Rwizile, wakati shauri hilo lilipopelekwa kwa kutajwa.

Washtakiwa walimkataa Hakimu Mmbando,  wakidai  kuwa hawana imani naye kwa madai kuwa haki yao inapotea.

Hakimu Mmbando alijiondoa kusikiliza kesi hiyo, Juni 4, 2019, wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutajwa.

Pia Soma

Kutokana na madai hayo, hakimu  Mmbando alijiondoa katika kesi hiyo na jalada la kesi hiyo lilipelekwa kwa Hakimu  Mfawidhi wa mahakama hiyo, Kelvin Mhina kwa ajili ya kupangiwa hakimu mwingine.

Hata hivyo jana, wakili wa Serikali Saada Mohamed aliieleza mahakama mbele ya Hakimu Mwandamizi, Augustine Rwizile  kuwa jalada halisi la kesi hiyo bado hajalipata lilikuwa kwa Hakimu  mwingine.

Saada baada ya kueleza hayo, Hakimu Rwizile alimtaka wakili huyo kuhakikisha analifuatilia kusudi tarehe ijayo awe na majibu ya kuifahamisha mahakama shauri lilipofikia.

Hakimu Rwizile aliahirisha kesi hiyo hadi Julai Mosi, 2019 itakapotajwa na washitakiwa walirudishwa rumande.

Katika kesi ya msingi, washitakiwa hao kwa pamoja wanakabiliwa na shitaka la mauaji ambapo  inadaiwa kuwa Novemba 3, mwaka 2013, walifanya kosa la mauaji ya kukusudia kinyume na kifungu cha 196 cha sheria na kanuni ya adhabu sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Ilidaiwa kuwa siku hiyo ya tukio, katika eneo la Msakuzi Kiswegere  lililoko eneo la Wilaya ya Kinondoni, washitakiwa hao kwa pamoja walimuua kwa kukusudia Dk. Sengondo Mvungi ambaye mjumbe  wa Katiba Mpya.

Chanzo: mwananchi.co.tz