Dar es Salaam. Kesi ya kuendesha mtandao ambao haujasajiliwa nchini kwa kikoa cha .co.tz (Tanzania domain) inayomkabili mkurugenzi mtendaji wa Jamii Media, Maxence Melo na mwenzake Micke William, imekwama kusikilizwa katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu.
Kesi hiyo ya jinai namba 458 ya mwaka 2016 ilipaswa kuendelea na ushahidi leo Jumatano Julai 3, 2019 lakini upande wa mashtaka hawakuwa na shahidi.
Wakili wa Serikali, Daisy Makakala amedai shahidi aliyepaswa kutoa ushahidi hakuwepo mahakamani, kuomba tarehe nyingine kwa ajili kuendelea na ushahidi.
Kutokana na maelezo hayo hakimu mkazi mkuu wa mahakama hiyo, Huruma Shahidi ameutaka upande wa mashtaka kuleta mashahidi mahakamani hapo ili kesi hiyo iweze kuisha na kuiahirisha hadi Agosti Mosi, 2019.
Katika Kesi ya msingi washtakiwa wanadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Desemba 9, 2011 na Desemba 13, 2016 katika eneo la Mikocheni wilayani Kinondoni.
Washtakiwa wanadaiwa kuendesha mtandao ambayo haujasajiliwa nchini yaani .tz (Tanzania domain) na kushindwa kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kuzuia taarifa binafsi za wateja wa mtandao wake.