Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA Bara Tundu Lissu ameonesha kutokukubaliana na utaratibu uliopo Mahakamani leo wa Watu mbalimbali kuzuiwa kuingia na simu za mkononi kufuatilia kesi ya Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe na wenzake watatu.
Lissu ameandika ujumbe kupitia mtandao wa Twitter, akilitaka Jeshi la Polisi kutenda haki, na kamwe haki haipatikani gizani.
“Nimetaarifiwa kwamba Polisi na/au Mahakama wanazuia watu kuingia na simu mahakamani ili kudhibiti utoaji wa taarifa za yanayoendelea kwenye kesi ya uongo dhidi ya Mwenyekiti Mbowe. Haki lazima ifanyike na ionekane imefanyika. Haki haiwezi kufanyika gizani na ikaonekana imefanyika,” ameandika Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu lissu
Baada ya mvutano kuwa mkubwa, polisi wamewaruhusu waandishi wa habari 10 kuingia na baadhi ya ndugu wa watuhumiwa. Hata hivyo imeelezwa kwamba walioingia mahakamani humo wametakiwa kuacha simu zao nje.
Mashahidi wanaotakiwa kutoa ushahidi wao leo ni pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Boaz na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Ramadhani Kingai.