Musoma. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Mara nchini Tanzania inamshikilia Katibu wa Msikiti wa Rahman uliopo Nyakato manispaa ya Musoma mkoani humo kwa tuhuma za kujifanya kamanda wa Takukuru mkoa wa Mara.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa Septemba 6, 2019 Mkuu wa Takukuru mkoa wa Mara, Alex Kuhanda amemtaja mtuhumiwa huyo ni Shaban Mohamed Kalla (30).
Amesema mtuhumiwa huyo kwa muda mrefu amekuwa kujihusisha na vitendo vya utapeli huku akijifanya ni Mkuu wa Takukuru mkoani Mara na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.
Amesema mbali na kujipatia fedha hizo lakini mtuhumiwa huyo amekuwa akiwatumia ujumbe mfupi wa simu watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa Serikali na wa kisiasa akiwahadaa kuwa wanatakiwa kufika ofisini Takukuru kwaajili ya mahojiano.
"Viongozi wengi wamefika hapa wakiwemo viongozi wa dini, mkurugenzi mtendaji wa halmashauri moja ya hapa pamoja na mwenyekiti wa chama cha siasa kutoka wilaya moja, wote hao walifika baada ya kutumiwa ujumbe mfupi na huyu jamaa huku akiwataka wafike chumba namba 13 ili kukutana na maofisa wangu" amesema Kuhanda
Amesema baada ya kupata taarifa hizo waliweza kuweka mtego na kufanikiwa kumkamata ambapo baada ya kufanya upekuzi nyumbani kwake walikuta line saba za simu pamoja na simu tano tofauti tofauti.
Pia Soma
- Kilichotokea kesi ya kigogo wa Takukuru hiki hapa
- VIDEO: Polisi Arusha yakamata 13 kwa tuhuma za uhalifu
- Maajabu tisa ya msitu wa Amazon
Aidha Kuhanda ameongeza kuwa ofisi yake hivi sasa inafanya uchunguzi juu ya tuhuma za viongozi wa kidini mkoani Mara kujihusisha na vitendo vya rushwa kwa maelezo kuwa malalamiko yamekuwa mengi na kuahidi kutoa taarifa baada ya uchunguzi kukamilika.