Sengerema. Zaidi ya Sh600,000 zilizotengwa kwa ajili ya malipo ya ankara ya maji katika ofisi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Nyampulukano, wilayani Sengerema zimezua jambo baada ya katibu wa kata hiyo kusimamishwa kazi akidaiwa kuzitafuna.
Hata hivyo, katibu huyo, Antony Busumabu amekana kutumia fedha hizo kwa shughuli binafsi, badala yake ameiambia Mwananchi kuwa zilitumika kwenye vikao vya kimkakati vya kuikomboa kata hiyo kutoka mikononi mwa Chadema.
“Tuhuma zinatokana na makundi ya kisiasa kwa sababu viongozi wanafahamu fedha zile zilitumika kurejesha udiwani kata ya Nyampulikano,” alisema.
Mwenyekiti wa CCM Kata ya Nyampulukano, Lugega Festo alidai katibu hiyo alikiri kutumia fedha hizo na aliahidi kuzirejesha.