Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kampuni yadaiwa ‘kupaki’ maziwa yaliyokwisha muda

8a934111db8e110598283e5ad86119f2 Kampuni yadaiwa ‘kupaki’ maziwa yaliyokwisha muda

Sun, 17 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

BODI ya Maziwa nchini imekamata zaidi ya kilo 3,600 za maziwa ya unga aina ya 'Cowbell' yanayodaiwa kuisha muda wake.

Aidha imebainika kuwa wamiliki wake wamekuwa wakiyafungasha upya katika vifungashio vingine na kuyaingiza tena sokoni.

Akizungumza kwenye ghala linalohifadhi maziwa hayo linalomikiwa na kiwanda cha Hawii, Keko jijini Dar es Salaam, Kaimu Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini, Noel Byamungu alisema kubainika kwa bidhaa hiyo kumetokana na ukaguzi unaoendelea kufanywa na bodi hiyo.

Byamungu alisema chunguzi waliofanya ulibaini kuwa maziwa hayo yalikwisha muda wake mwishoni mwa mwaka uliopita hivyo kutokana na hatua hiyo, wamiliki hao waliyatoa katika makopo ambayo yameonesha muda wake kuisha na kuyajaza katika vifungashio vingine na kugonga tarehe mpya za matumizi.

"Kitendo kinachofanywa na wamiliki hawa ni kinyume na utaratibu wa bodi ya maziwa kwa kuwa kinaweza kuhatarisha afya ya mlaji, hivyo kutokana na sheria na taratibu zetu tunakifungia kiwanda hiki kuendelea na uzalishaji hadi pale uchunguzi unaoshirikisha mamlaka mbalimbali utakapokamilika," alisema Byamungu.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Athumani Kisumo, alisema wanakwenda kufanya uchunguzi wa maziwa hayo kujiridhisha ubora wake baada ya kubainika kwa kitendo hicho ambacho ni kinyume cha sheria na taratibu za ubora wa bidhaa za vyakula.

Alisema kwa kutumia maofisa wa mamlaka hiyo, wanakusudia kufanya uchunguzi wa kina wa bidhaa hizo kwa lengo la kubaini kama kweli wamiliki wake wametenda hicho kitendo ili hatua zaidi ziweze kufuata mkondo wake kulingana na kanuni, sheria na taratibu za viwango ubora na ubora wa bidhaa vinavyosimamiwa na mamlaka hiyo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Temeke, Amon Kakwale alisema jeshi hilo linawashikilia watu wawili kutoka katika kiwanda hicho akiwamo meneja uzalishaji. Hata hivyo majina yao hakuyataja kutokana na uchunguzi unaoendelea.

Alisema ikibainika kuwa watu hao wametenda kosa hilo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao kwa kuwafikisha mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.

Kwa upande wake, Msemaji wa Kiwanda hicho Marygoreth Faustine alikanusha kuwa kiwanda hicho kilikuwa kinabadilisha vifungashio na kurejesha sokoni maziwa hayo.

Alisema kilichokuwa kikifanyika ni utaratibu wa kawaida ya uwekeaji wa maziwa katika vifungashio kama ilivyo kawaida yaweze kupelekwa sokoni.

Alisema kwa kuwa suala hilo kwa sasa lipo katika uchunguzi wa mamlaka zinazohusika, wanaliacha hadi utakapokamilika na mamlaka hizo kujiridhisha ili kuendelea na taratibu zingine.

Chanzo: habarileo.co.tz