Mwanza. Utata umeendelea kugubika tukio la mtu asiyejulikana aliyekutwa amekufa eneo la Hoteli ya Kitalii ya Gold Crest jijini Mwanza baada ya kamera za ulinzi (CCTV) kuonyesha kuwa alijirusha kutoka ghorofa ya nne ya hoteli hiyo.
Hata hivyo, msimamizi wa idara ya ulinzi wa jengo la hoteli hiyo yenye ghorofa kumi, Benard Kakongo ameiambia Mwananchi leo Mei 14, 2019 kuwa hakuna kamera iliyomnasa mtu huyo wakati akiingia eneo hilo.
“Tumeshakabidhi picha zilizonasa tukio hilo kwa polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi,” amesema Kakongo.
Akijibu swali kwa nini kamera hizo zinase tukio la kujirusha pekee bila kuonyesha mtu huyo akiingia, mkuu huyo wa idara amesema yawezekana alitumia njia ya kuingia na kutoka magari na ile ya wafanyakazi ambayo haikuwa na kamera za ulinzi.
“Watu wote wanaoingia na kutoka kupitia lango kuu hukaguliwa kwa mashine maalum na kunaswa na kamera za ulinzi ambazo pia zinachukua matukio yote yanayotokea kuzunguka jengo isipokuwa ile njia ya kuingia na kutoka magari,” amesema.
Kakongo amesema hadi sasa uchunguzi wa kina umebaini kuwa mtu huyo anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 25 hadi 30 hakuwa mmoja wa wapangaji wala wateja wa hoteli hiyo inayopokea wageni na wateja wa aina mbalimbali.
Pia Soma
- Magereza Tabora kuzalisha bidhaa za ngozi
- Mbunge CCM ataka mawaziri waachie ngazi
- Mbunge akerwa Serikali kutotoa fedha kwa wakati
- Kesi ya Maimu, wenzake yapigwa kalenda