SHAHIDI wa tisa katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya (34) na wenzake sita leo (Jumatatu) anatarajiwa kutoa ushahidi kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha.
Katika kesi hiyo inayosikilizwa na Hakimu, Patricia Kisinda, Sabaya na wenzake wanakabiliwa na mashitaka manne.
Mara ya mwisho shahidi wa saba ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama), Kanda ya Kaskazini katika Benki ya CRDB, Godfrey Nnko alimaliza ushahidi wake.
Hata hivyo, ushahidi wake ulisitishwa kumpisha shahidi wa nane, Johnson Kisaka. Shahidi huyo ni Ofisa Uchunguzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Katika mchakato wa ushahidi, awali zilioneshwa video sita zilizorekodiwa Januari 22 mwaka huu katika Benki ya CRDB, Tawi la Kwa Mrombo jijini Arusha.
Awali, shahidi wa nane, Kisaka alidai wakati anatoa video hizo kwa maofisa wawili wa (Takukuru) alikuwa na Meneja wa Tawi la CRDB Kwa Mrombo, Mery Kisamu lakini hakujaza fomu yoyote kuonesha kuwa alitoa video hizo sita kwa maofisa hao.
Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Enock Mnkeni {41), Watson Mwahomange (27) maarufu kwa jina la Malingumu, John Aweyo (45), Syliverster Nyengu (26), Jackson Macha (29) na Nathan Msuya (31).