Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kushirikiana na Maafisa Madini Wilaya ya Chunya limefanikiwa kukamata madini aina ya dhahabu yenye thamani zaidi ya Tsh milioni mia arobaini (140).
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ulrich Matei, ameeleza kuwa Februari 9, 2022 majira ya saa 19:30 usiku katika kizuizi cha Polisi Chalangwa kilichopo Kata ya Chalangwa, Tarafa ya Kiwanja, Wilaya ya Chunya, Mkoa wa Mbeya, Askari Polisi kwa kushirikiana na Maafisa Madini Wilaya ya Chunya walikamata Gari T.948 DTM aina ya Toyota Crown iliyokuwa ikiendeshwa na mtu aliyefahamika kwa jina BARAKA SINGU NYODA, ambaye baada ya kusimamishwa kwenye kizuizi hicho alikimbia na kutelekeza gari hiyo.
Katika upekuzi uliofanywa kwenye gari hiyo vilikutwa vipande 36 vya madini aina ya dhahabu vyenye uzito wa gramu 1367.07 vyenye thamani ya Tshs. 147,694,961.83/= na fedha taslimu Tshs. 504,600/=, lengo ni kukwepa kodi na tozo za serikali.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linaendelea na msako wa kumtafuta mtuhumiwa kwa hatua zaidi za kisheria.
Aidha, linatoa rai kwa wafanyabiashara kutambua kuwa mkono wa serikali ni mrefu hivyo ni vyema kufanya biashara halali kwa kufuata sheria na taratibu zilizopo ili kuepuka kukinzana na sheria.