Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Jeshi la Polisi kuanzisha Mradi wa Mahakama ya watoto

Mutafungwa.jpeg Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani akizungumza wakati wa uzinduzi

Tue, 1 Mar 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Jeshi la Polisi kikosi cha Usalama barabarani kwa kushirikiana na Shirika lisilo la kiserikali la Amend wamezindua mradi wa usalama barabarani kwa shule za msingi za serikali jijini Dar es Salaam ujulikanao kama ‘Mahakama ya Watoto’ utakaohusisha utoaji wa elimu ya usalama barabarani kwa zaidi ya wanafunzi 11,000.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, SACP Wilbroad Mutafungwa amesema mradi huo utatoa kipaumbele kwa shule zenye wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Amesema kuwa kwa mujibu wa Shirika la Afya duniani (WHO) linakadiria kuwa watu takriban 3,700 hufariki kila siku kwa ajali za barabarani duniani kote, huku Afrika ikiwa na idadi kubwa zaidi ya majeruhi watokanao na inaongezeka kila mwaka kutokana na kukua kwa kasi ya maendeleo.

“Nchini Tanzania takwimu zinaonesha kwa kipindi cha mwaka 2021, watu 1,245 walipoteza maisha na wengine 2,023 walijeruhiwa kutokana na ajali za barabarani. Taarifa zinaonesha kuwa jumla ya wanafunzi 56 walipoteza maisha na wengine 65 kujeruhiwa katika ajali hizo.

“Mwaka huu katika kuendelea kutoa elimu ya usalama barabarani kwa makundi mbalimbali nchini, Jeshi la polisi kikosi cha usalama barabarani tukishirikiana na Amend tutaendesha mradi huu wa Mahakama ya Watoto...

"Ambao utahusisha kutoa elimu na mahojiano maalum ambayo yanafanywa kati ya wanafunzi na madereva watakaobainika kuvunja sheria za usalama barabarani kwenye maeneo ya shule hizo,” amesema Kamanda Mutafungwa.

Aidha Kamanda Mutafungwa aliwataja waathirika wakuu wa ajali za barabarani kuwa ni watembea kwa miguu, waendesha pikipiki na bajaji, watoto wadogo wanaopandisha mshikaki kwenye pikipiki pamoja na madereva wa magari ambao hawazingatii sheria za usalama barabarani.

Kwa upande wake Meneja Mkuu wa Amend, Simon Kalolo amefafanua mradi huo utahusisha shule 10 za Jiji la Dar es Salaam zenye uhitaji na kwamba mafunzo hayo yatawasaidia wanafunzi hao kutoa elimu ya usalama barabarani moja kwa moja kwa madereva.

"Na baada ya kukamilisha mradi huu tutatoa vyeti vya kuwatambua washiriki wote,” alisema Kalolo.Mradi wa namna hii ambao tunauzindua leo ulishawahi kutekelezwa mwaka 2019 na 2020 jijini Dar es Salaam na baadae mkoani Tanga mwaka 2021.

“Tuna shule nyingi ambazo Serikali imeweka alama maalum lakini wengine hawazifahamu na wengine hawaoni umuhimu wa kuzitumia, kwahiyo kupitia mradhi huu tutawaelimisha,” amesema Kalolo huku akisisitiza ni muhimu kwa jamii ya Watanzania kushirikiana kikamilifu katika kuchukua hatua madhubuti kukomesha ajali za barabarani.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live