Siha. Mahakama ya Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro imemhukumu kifungo cha miaka 60 jela Abrahamu Kaaya (23) mkazi wa kijiji cha Karansi wilayani Siha kwa makosa mawili ya kubaka na kumpa ujauzito mwanafunzi wa kidato cha kwanza Shule ya Sekondari Karansi.
Hukumu hiyo imetolewa leo Jumatatu Oktoba 22, 2018 na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo Jasmine Abdul baada ya kuridhika na ushahidi wa mashahidi watano.
Mwendesha mashtaka wa Serikali, Simoni Feo amedai mahakamani hapo kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Oktoba 11, 2017 katika kijiji hicho.
Mwendesha mashtaka huyo aliomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali dhidi ya mshtakiwa kutokana na kukithiri kwa vitendo hivyo ili iwe fundisho kwa watu wenye tabia kama hiyo.