Tabora. Wakazi wawili wa kijiji cha Loya wilayani Uyui mkoani Tabora, Lubasha Masanja na Shimiyu Masenga, wamehukumiwa kifungo cha maisha baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka msichana wa miaka 14.
Watu hao wamehukumiwa na hakimu mkazi mfawidhi mkoa wa Tabora, Chiganga Tengwa kutokana na kuridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka.
Wakili wa Serikali, Tito Mwakalinga, ameiambia mahakama kuwa washitakiwa walitenda kosa hilo tarehe 3 Novemba mwaka jana baada ya awali kutaka kumpa lifti binti huyo lakini alikataa.
Amezidi kuieleza mahakama kuwa walipokataliwa walimvizia kwenye msitu na kisha kumbaka mlalamikaji ambaye ni binti wa miaka 14.
Hakimu Chiganga alikubaliana na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka na kuwahukumu kifungo hicho.