Dar es Salaam. Upande wa mashtaka katika kesi ya mauaji inayomkabili Ramadhan Mlaku (28) askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania ( JWTZ) umeieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa jalada la kesi hiyo limeshawasilishwa katika ofisi ya mwendesha mashtaka (DPP) kwa ajili ya kulitolea uamuzi.
Wakili wa Serikali ya Tanzania, Sylivia Mitanto amedai hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba leo Jumatatu Julai 1, 2019 kuwa upelelezi bado haujakamilika hivyo jalada limewasilishwa katika ofisi ya mwendesha mashtaka tangu Aprili 8, 2019 kwa ajili ya kutolea uamuzi.
"Jalada limeshaletwa ofisini kwetu kwa ajili ya kutolea uamuzi tangu Aprili 8,2019 bado mapema sana kulitolea uamuzi shauri hili," amedai Mitanto.
Hakimu Simba amesema upande wa mashtaka wahakikishe wanalifuatilia ili shauri hilo liweze kwenda mbele kwa kuwa jalada limeshawafikia tangu Aprili mwaka 2019.
Shauri hilo limeahirishwa hadi Julai 15, 2019 itakapotajwa tena.
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, Mlaku anadaiwa kutenda kosa hilo Oktoba 30, 2017, eneo la Upanga, makao makuu ya Jeshi hilo.
Pia Soma
- Samia kufungua maonyesho ya 43 ya sabasaba
- Mikoa minane kusini Tanzania yashirikiana kutangaza utalii
- Daktari atoa ushahidi kesi ya Mbowe na wenzake, ataja kitu cha ncha kali