Arusha. Mahakama ya hakimu mkazi wilaya ya Arusha, Desemba 3,2018 inatarajiwa kusoma hukumu ya kesi ya mwalimu Joel Mbaga (28) anayetuhumiwa kumlawiti mwanafunzi wa kiume kidato cha kwanza mwenye umri wa miaka (13) katika shule ya Adili iliyopo mkoani Arusha.
Hakimu wa mahakama ya wilaya ya Arusha, Patricia Kisinda, ametoa uamuzi huo, leo Novemba 5,2018 baada ya mashahidi wawili upande wa utetezi, Mwalimu Mbaga na Mlezi wa wanafunzi, Dionisia Asenga kukamilisha kutoa ushahidi wao.
Katika ushahidi wao, mashahidi hao, wote walieleza mwanafunzi huyo, alitoa taarifa kwa maandishi kuingiliwa na popobawa akiwa shuleni na sio kulawitiwa kama ambavyo baadaye taarifa zilipatikana.
Katika kesi hiyo, Wakili wa Serikali, Naomi Mollel alisema Mwalimu Mbaga anatuhumiwa kutenda kosa hilo kati ya Septemba na Oktoba mwaka jana shuleni hapo, wakati akijua ni kinyume cha sheria.