Mtwara. Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara inatarajia kutoa hukumu ya kesi ya kupinga matumizi ya kanuni za maudhui ya kimtandao Januari 9, 2019.
Kesi hiyo namba 25 ya mwaka 2018 ilifunguliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC)na Muungano wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu wote kwa pamoja wanapinga kanuni za maudhui ya kimtandao.
Katika kesi hiyo washtakiwa ni Waziri wa Habari, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Mwanasheria Mkuu.
Leo Alhamisi Desemba 13, 2018 hukumu ya kesi hiyo ilipangwa kutolewa lakini upande wa wajibu maombi waliwasilisha pingamizi kwamba ada ya Mahakama iliyolipwa na wapeleka MCT, kituo cha sheria na haki za binadamu na Muungano wa Mtandao wa watetezi wa haki za binadamu ni pungufu.
Jaji Wilfread Ndyansobera amesema kufuatia mapingamizi yaliyowekwa na upande wa wawajibu maombi, waombaji hawakuwa na makosa kulipa ada pungufu na badala yake walilipa ada waliyotakiwa na mahakama ambayo ni Sh55,000 badala ya Sh100,000
Jaji Ndyansobera ametoa maagizo kwa wapeleka maombi hao kuhakikisha wanalipa ada iliyosalia ndani ya siku mbili kwani ni kodi ya Serikali.
Kwa kawaida kanuni hizo zilipaswa kuanza kutumika rasmi Mei 5 mwaka huu lakini Mei 4 mwaka huu, Mahakama hiyo iliweka zuio la muda baada ya kuwasilishwa kwa shauri la kupinga.