Mbozi. Hukumu ya mbunge wa Mbozi (Chadema) Paschal Haonga na wenzake wawili, imeahirishwa hadi Agosti 10 mwaka huu.
Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi, Wilaya ya Mbozi, Nemes Chami, amesema mahakamani hapo leo Julai 10, kuwa kutokana na unyeti na uzito wa shauri hilo, bado anahitaji muda wa kutoa hukumu hiyo.
Amesema kuwa pia ana majukumu mengi mahakamani hapo.
Haonga na wenzake, Wilfredy Mwalusanya (katibu wa Haonga) na Mashaka Mwampashi wanakabiliwa na makosa matatu.
Makosa hayo ni pamoja na kuvuruga mkutano wa uchaguzi wa Baraza la mji mdogo wa Mlowo na kosa la pili na tatu ni kuwazuia askari kutekeleza majukumu yao na wanadaiwa kutenda makosa hayo Agosti 28 mwaka jana.
Wabunge waliofika mahakamani hapo ni pamoja na Sophia Mwakagenda wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya,(Chadema) Mbunge wa Tunduma, Frank Mwakajoka, Meya wa Tunduma, Ally Mwafongo, Katibu wa Chadema Kanda ya Nyasa, Emmanuel Masonga na viongozi wengine Chadema.