Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam nchini Tanzania imepanga kutoa hukumu katika kesi inayomkabili Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jamii Forum, Maxence Melo na mwenzake Micke William Januari 22, 2020.
Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba amesema leo Ijumaa Desemba 6, 2019 wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa lengo la kupangiwa tarehe ya hukumu.
Awali, Wakili wa Serikali ya Tanzania, Sylvia Mitanto aliieleza mahakama hiyo kuwa kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya kusomewa hukumu.
Hukumu hiyo inatarajiwa kutolewa na Hakimu Simba baada ya kusikiliza ushahidi wa mashahidi wanne wa upande wa mashtaka pamoja na ushahidi wa upande wa utetezi uliotolewa na washtakiwa wenyewe.
Melon na Willium wanadaiwa kuzuia Jeshi la Polisi nchini Tanzania kufanya uchunguzi kinyume cha Sheria namba 22 (2) cha Sheria ya Makosa ya Mtandano Namba 14 ya mwaka 2015.
Washtakiwa hao wanadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Aprili Mosi, 2016 na Desemba 13, 2016 katika maeneo ya Mikocheni wilayani Kinondoni, Dar es Salaam nchini Tanzania.