JESHI la Polisi Mkoa wa Mwanza linamshikilia mfanyakazi wa ndani, Ashura Suka kwa tuhuma za kumuua mtoto mdogo wa mwajiri wake.
Akizungumza na HabariLEO jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro alisema tukio hilo lilitokea Agosti 23 mwaka huu majira ya 10:30 usiku kata ya Iloganzala wilayani Ilemela.
Alisema mtoto mwenye umri wa miezi 11, Kelvin Kastus, mkazi wa Iloganzala, aliuawa kwa kuzibwa pumzi kwa kutumia shuka na mfanyakazi huyo wa ndani mwenye miaka 15 ambaye ni mkazi wa Nyamanoro.
Muliro alisema chanzo cha mauaji hayo kinachunguzwa kwa kina na upelelezi utakamilishwa haraka kadri iwezekanavyo ili mtuhumiwa afikishwe mahakamani. Mwili wa marehemu umehifadhiwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Sekou Toure kwa uchunguzi wa daktari.
Aliwataka wazazi na walezi wenye watoto wadogo kujenga utamaduni wa kuajiri watu wanaowafahamu tabia, mienendo na malezi kwani ni hatari kumwachia mtu usiyemfahamu vizuri afanye kazi ya malezi ya mtoto mdogo.