Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Halima Mdee: Sikushiriki maandamano

87271 Halimamdeepic Halima Mdee: Sikushiriki maandamano

Thu, 5 Dec 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Halima Mdee, mshtakiwa wa saba katika kesi inayowakabili viongozi tisa wa Chadema akiwemo mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa hakuwahi kushiriki maandamano.

Mbunge huyo wa Kawe ameeleza hayo leo Alhamisi Desemba 5, 2019 wakati akitoa ushahidi katika kesi ya jinai namba 112/2018 yenye mashtaka 13 yakiwemo ya uchochezi inayomkabili pamoja na wenzake.

Mdee akiongozwa na wakili  wa utetezi, Peter Kibatala amedai kuwa Februari 16, 2018 kabla ya mkutano wa kufunga kampeni za uchaguzi wa marudio jimbo la kinondoni alikuwa bungeni Dodoma.

Amedai  kuwa siku hiyo afya yake haikuwa nzuri na alishiriki mkutano huo kuonyesha mshikamano na upendo kwa mgombea na baada ya kushuka  jukwaani aliondoka.

"Nilifika Dar es Salaam saa 5 asubuhi  na kwenda kwenye mkutano saa tisa alasiri. Baada ya kuhutubia niliondoka kwa kuwa nilikuwa naenda kujiandaa na safari,” amesema Halima.

Akijitetea mbele ya  Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, mbunge huyo amesema alikamatwa na askari katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) akiwa anatokea Afrika Kusini kwenye matibabu.

Alipoulizwa na Kibatala maneno aliyozungumza jukwaani yalikuwa yana dhana gani, alijibu alikuwa akimuombea kura mgombea ubunge, Salum Mwalimu.

Akizungumzia maneno aliyotamka jukwaani amesema alieleza changamoto mbalimbali kama kufukuzwa bungeni, watu kupotea na wafanyabiashara kufilisiwa.

Chanzo: mwananchi.co.tz