Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeshindwa kuendelea na kesi inayomkabili mwandishi wa habari, Erick Kabendera kutokana na hakimu anayesikiliza kutokuwepo mahakamani.
Akizungumza leo Alhamisi Oktoba 24, 2019 mbele ya Hakimu mkazi, Vick Mwaikambo wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon amedai kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya kutajwa na upelelezi bado haujakamilika.
Simon amedai shauri hilo linasikilizwa mbele ya Hakimu Mkazi mwandamizi, Augustine Rwizile ambaye hakuwepo mahakamani hapo na kuomba kesi kuahirishwa.
Baada ya maelezo hayo kesi hiyo iliahirishwa hadi Novemba 7, 2019.
Oktoba 11, 2019 Kabendera aliieleza mahakama hiyo kuwa anataka kujadiliana na mkurugenzi wa mashtaka nchini (DPP) namna ya kumaliza kesi inayomkabili.
Jebra Kambole, wakili wa Kabendera siku hiyo alidai mteja wake anataka kujadiliana na DPP namna ya kumaliza kesi inayomkabili kwa mujibu wa kifungu namba 194A(2) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2019.
Habari zinazohusiana na hii
- Erick Kabendera kuanza majadiliano na DPP
- Erick Kabendera amuomba msamaha Rais
- VIDEO: Kabendera: Nimefanyiwa kipimo cha X Ray, damu
- VIDEO: Mahakama yaelezwa Erick Kabendera hapumui vizuri
Katika shtaka la pili, inadaiwa siku na mahali hapo mshtakiwa bila kuwa na sababu za msingi kisheria alishindwa kulipa kodi ya Sh173.24 milioni ambayo ilitakiwa ilipwe kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Katika shtaka la utakatishaji fedha, kati ya Januari 2015 na Julai 2019 ndani ya jiji na mkoa wa Dar es Salaam mshtakiwa alijipatia kiasi hicho cha Sh173.2 milioni wakati akizipokea alijua kuwa fedha hizo ni mazao ya makosa tangulizi ya kukwepa kodi na kujihusisha na genge la uhalifu.