Mwenyekiti wa Halmashauri wa Wilaya ya Morogoro, Lucas Lemomo, amehukumiwa kifungo cha miezi sita jela baada ya kupatikana na hatia ya kuingiza mifugo kwenye mashamba na kuharibu mazao ya wakulima.
Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo, Tarafa ya Ngerengere, Godfrey Ng'itu, ameridhika kuwa mwezi Agosti mwaka huu mshtakiwa aliingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima watatu kwa makusudi na kuharibu mazao yao.
Ushahidi unaonesha kuwa moja ya shamba aliloharibu mshitakiwa huyo ambaye ni mfugaji wa jamii ya kimasai ni lenye mboga aina ya matembele na mahindi, vyote vikiwa na thamani ya Sh79,000.
Mfugaji huyo alidaiwa pia kuharibu shamba la mkulima mwingine lilikuwa na mahindi, kunde na mbaazi vyenye thamani ya Sh240,000.