Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Dhamana ya mwandishi wa habari Tanzania kujulikana Agosti 5

69265 KABDENDERA+PIC

Thu, 1 Aug 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar  es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam nchini Tanzania imepanga Agosti 5, 2019 kusikiliza maombi ya dhamana ya Mwandishi wa habari za uchunguzi, Erick Kabendera.

Uamuzi huo umetolewa leo Alhamisi, Agosti Mosi,2019 na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama hiyo, Augustine Rwizile, baada ya upande wa mashtaka kuomba Mahakama hiyo kuleta kiapo kinzani.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon amedai mahakamani hapo kuwa upande wa mashtaka wamepokea maombi hayo leo Alhamisi hivyo  wanaomba muda wa kuyapitia na kuwasilisha hati kinzani.

Uamuzi wa kusikiliza shauri hilo, Jumatatu ijayo, unatokana na Maombi  ya dhamana namba 14/ 2019  yaliwasilishwa jana Mahakamani hapo na Wakili wa kutoka Mtandao wa Utetezi wa Haki za binadamu, Shilinde Swedy.

Katika maombi hayo, Swedy anaomba mteja wake ambaye ni Kabendera apatiwe dhamana au afikishwe mahakamani.

Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Hakimu Rwezile  aliahirisha shauri hilo hadi Agosti 5, 2019, ambapo mahakama hiyo itasikiliza maombi ya dhamana ya upande wa utetezi.

Habari zinazohusiana na hii

Kabendera anashikiliwa na Idara ya Uhamiaji nchini Tanzania tangu Julai 29, 2019 baada ya kuchukuliwa kwa nguvu na Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam nyumbani kwake, Mbweni jijini Dar es Salaam.

Baada ya kuchukuliwa, mwandishi huyo anayeandikia magazeti ya ndani na nje ya Tanzania amekuwa akihojiwa kuhusu uraia wake ambapo jana Jumatano, Idara ya Uhamiaji ilikwenda kufanya upekuzi nyumbani kwake, Mbweni na kufanikiwa kuchukua paspoti saba ambapo moja ni ya kwake zingine za ndugu zake.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz