Dereva wa Mbunge wa Likuyani, Enock Kibunguchy ameuawa kwa kupigwa risasi akiwa amejipumzisha hotelini eneo la Kakamega nchini Kenya.
Shambulio hilo lilitokea jana saa tatu usiku wakati mbunge huyo aliposimamisha gari yake katika hoteli hiyo ili kujiburudisha akiwa na dereva wake huyo.
Inasadikika kuwa lengo la shambulio hilo lilikuwa kwa Mbunge lakini kwa bahati mbaya aliyefyatuliwa ni dereva na alipoteza maisha papo hapo.
Mwili wa marehemu ulipelekwa kuhifadhiwa katika Hospitali ya Moi iliyopo Eldoret nchini humo.
Polisi mkuu msaidizi ukanda wa Magharibi, Chief Leonard Omolo alisema majambazi walifyatua gari hilo wakati Kibunguchy alipokuwa akijiandaa kutoka nje ya gari.
“Kwa bahati mbaya, bado mbunge huyo alikuwa ndani ya gari wakati shambulio lilipotokea. Hakujeruhiwa lakini tunasadiki kuwa yeye ndio alikuwa lengo la shambulio hilo,” alisema Omolo.