Pemba. Mamlaka ya kuzuia rushwa na uhujumu uchumi Zanzibar (ZAECA) inamshikilia, Dk Massoud Suleiman Abdalla wa Hospitali ya Chakechake kwa madai kuomba rushwa ya ngono kwa mjamzito.
Inadaiwa daktari huyo aliomba rushwa hiyo kama fidia ya kumfanyia mjamzito huyo uchunguzi katika hospitali hiyo.
Mwanamke huyo alifanikisha kukamatwa kwa daktari huyo baada ya kuwasilisha malalamiko yake katika mamlaka hiyo na mtego kuandaliwa. Daktari huyo alikamatwa akitaka kumuingilia kimwili mwanamke huyo wakiwa chooni.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumamosi Novemba 23, 2019 ofisa wa mamlaka hiyo kisiwani Pemba, Suleiman Ame Juma amesema tukio hilo lilitokea juzi Novemba 21, 2019 saa 2 asubuhi.
Amesema walipopata taarifa ya mlalamikaji kukosa huduma kutoka kwa daktari huyo mpaka afanye naye ngono waliandaa mtego na kufanikiwa kumnasa.
“Tulimkamata baada ya kumuomba ofisa mmoja mwanamke kama shahidi. Aliomba kufunguliwa mlango wa chooni lakini alikataa (daktari), tulitumia nguvu kuufungua na kuwakuta wakiwa hawana nguo,” amesema Juma, kubainisha kuwa baada ya tukio hilo daktari huyo alikamatwa.