Dar es Salaam. Daktari kutoka Hospitali ya Amana, Yusuph Ally ameieleza Mahakama ya Wilaya ya Ilala jinsi alivyowafanyia uchunguzi watoto wawili kati ya watatu wa kike wanaodaiwa kubakwa na Ustadhi Salum Kingo (66) na kubaini kuwa waliingiliwa na kwamba hawakuwa na bikra.
Shahidi huyo wa upande wa mashtaka aliyaeleza hayo leo Jumatatu ya Juni 10 wakati akiongozwa na wakili wa Serikali, Anna Chimpae kutoa ushahidi mbele ya Hakimu Mkazi, Samweli Obasi.
Akitoa ushahidi mahakamani hapo, Dk Ally alieleza kuwa aliwafanyia vipimo watoto hao wawili wa kike wenye umri wa miaka 13 na 14 na mbali ya kubaini wameingiliwa, alibaini pia mtoto mmoja ameambukizwa ugonjwa wa zinaa wa kisonono.
Alieleza kuwa uchunguzi huo aliufanya Novemba 2, mwaka jana baada ya watoto hao kupelekwa hospitalini hapo na wazazi wao na baada ya kuwafanyia vipimo hivyo na kupata uthibitisho huo huo alijaza fomu namba tatu ya polisi PF3.
Baada ya kueleza hayo, shahidi huyo aliiomba mahakama kupokea PF3 hizo mbili kama vielelezo vya ushahidi katika kesi hiyo.
Hata hivyo baada ya kutolewa kwa ombi hilo na shahidi wa upande wa mashtaka, Ustadhi Salum alipinga na kuiomba mahakama isipokee PF3 kama sehemu ya ushahidi katika kesi hiyo.
Pia Soma
- VIDEO: Basungwa amuahidi Magufuli kuanza na blueprint
- MAUAJI YA MWANAFUNZI SCOLASTICA: Yaliyojitokeza mwanzo hadi mwisho kesi ya mauaji ya mwanafunzi Humphrey
- Magari 200 ya mchanga yapata vibali
- MAUAJI YA MWANAFUNZI SCOLASTICA: Aliyehukumiwa kunyongwa mauaji Scolastica akata rufaa
Akijibu hoja hiyo ya Ustashi Salum, shahidi huyo wa upande wa mashtaka alidai kuwa yeye alipelekewa watoto tu kuwapima na akawapima.
Mshtakiwa huyo Ustashi Salum aliendelea kumuhoji shahidi kuwa yeye aliwafanyia vipimo na kubaini waliingiliwa je ana uthibitisho gani kuwa yeye ndiyo aliwaingilia.
Akijibu hoja hiyo, shahidi huyo alidai kuwa yeye aliwafanyia vipimo na kuthibitisha waliingiliwa, waliingiliwa na nani yeye hajui.
Baada ya kuelezwa hayo na mengine, wakili wa serikali Chimpae aliiomba mahakama kutupilia mbali mapingamizi ya mshtakiwa huyo kwa sababu hayana mashiko kwa mujibu wa sheria.
Hakimu Obasi alikubaliana na maelezo ya upande wa mashtaka na kupokea vielezo hivyo na kuiahirisha kesi hadi Juni 20 mwaka huu.