Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) nchini Tanzania, Biswalo Mganga amesema Serikali imeamua kufungua akaunti maalumu yenye lengo la kuwawezesha washtakiwa wanaoandika barua za kukiri makosa yao ya uhujumu uchumi na kuamriwa kurudisha fedha kulipia kwenye akaunti hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Oktoba 3, 2019 jijini Dar es Salaam, Mganga amesema akaunti hiyo maalum imefunguliwa Benki Kuu Tanzania (BoT) kwa amri ya Serikali ya Tanzania.
Amesema hakuna fedha itakayolipwa kwenye akaunti ya mahakama, ofisi ya Taifa ya Mashtaka au Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
“Ambaye atalipa kwingine huko tusilaumiane, lazima fedha ziende zinapotakiwa kwenda, si mawakili wa Serikali, si watumishi wa ofisi hii au mtu yeyote atakayefanya vitendo vya rushwa tutamvumilia,” amesema
DPP amefikia hatua hiyo baada ya kuwepo baadhi mawakili wanaochukua fedha kwa washtakiwa na kusema wanapeleka ofisini kwake ila hawafikishi.
Amewaonya kuacha tabia hiyo kwa sababu wanatafuta ugomvi.
Habari zinazohusiana na hii
- Kulthum Mansooor wa Takukuru amwandikia DPP barua ya kukiri makosa
- VIDEO: Mkanganyiko msamaha kwa wahujumu uchumi
Mkurugenzi huyo amesema, “wanaofanya hivyo wanatafuta ugomvi na tayari nimeanzisha uchunguzi wasije tukalaumiana, wafanye kazi zao za kiuwakili bila kuathiri heshima ya ofisi ya DPP.”
Mganga amesema watu wote wanaofanya uhalifu katika kipindi hiki cha washtakiwa walioambiwa kuomba msamaha kwa kuwaibia fedha zao kupitia ndugu au washtakiwa wenyewe waache.