Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Bweni lanusurika kuteketea kwa moto, Wazazi wacharuka

Plc Il Mkaguzi wa Polisi Josiah Ndulu akizungumza na wazazi

Tue, 22 Mar 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Bweni la hosteli ya wasichana la shule ya sekondari Kilimani, limenusurika kuteketea kwa moto baada ya jaribio linalodaiwa kufanywa na watu wenye nia ovu kuzimwa huku serikali na wazazi wakicharuka kuhusu tukio hilo la moto.

Tukio hilo lilitokea Machi 14, mwaka huu, majira ya saa 3:00 wakati wanafunzi wakiwa darasani wakijisomea ambapo watu kadhaa waliingia kwenye hosteli hizo na kuwasha moto kwenye moja ya vitanda vya bweni baada ya kuruka ukuta wa uzio.

Kutokana na tukio hilo Bodi ya shule ya Kilimani,wazazi,walimu na wanafunzi wa shule hiyo ya sekondari,wamelaani jaribio la kuchoma moto bweni la hosteli ya wasichana na kuliomba jeshi la polisi kufanya uchunguzi wa kina ili kuwabaini wahusika na kuwachukulia hatua za kisheria.

“Tukio hilo si la bahati mbaya,limefanywa kwa makusudi na watu wenye nia ovu kwa shule ya Kilimani,wanaoionea wivu kwa maendeleo yanayofanywa hapa yakiwemo ya kitaaluma na miundombinu,”alisema Mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo, Athanas Bagenyi.

Mmoja wa wazazi Getrude Ringo,alisema tukio hilo linaonyesha wapo majirani waliona na kuwaomba wasifichiane maovu na wasiwe na makundi,kama wanawafahamu waliofanya hujuma na tukio hilo ovu la kudhuru maisha ya watoto,dhamira zao ziwasute na kuwafichua.

“Tusimame kama wazazi,wananchi na jamii, shule hii si walimu ni yetu na vizazi vyetu, tukemee maovu tangu nyumbani kwa watoto wetu na kujenga nidhamu yao na maadili,vita iko masika na kiangazi na kwa tukio hili tusifichiane maovu na tusiwe na makundi kwa ajili ya maendeleo kuwa wapo wenye hela zao watafanya,kama mnao elimu ni ghali jaribuni ujinga,”alisema.

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Kawekamo,Elis Joseph, alisema madai kuwa tukio hilo limesababishwa na mgogoro kati ya shule na jamii si sahihi,suala hilo ni la kijinai serikali inalishughulikia.

“Watuhumiwa wanafahamika,ni watu wachache na wahuni wenye nia ovu wasio na uelewa,wanafanya kwa kivuli cha mgogoro,baada ya kujenga uzio waliibuka watu wakilalamika kuingiliwa kwenye ardhi yao, upimaji ukafanyika shule ikamilikishwa,wanajaribu kui-beep serikali,itawashughulikia,”alisema.

Mkuu wa Shule ya Kilimani, Majaliwa Gerana,alisema shule ni taasisi hivyo wasigombanishwe na jamii, ugomvi wao ni kupata matokeo chanya ya kitaaluma ukiwemo ufaulu mzuri wa wanafunzi na ujenzi wa mabweni ya wasichana.

Alisema kuna vikao vinafanywa kwenye nyumba ya serikali vya kupanga njama na hujuma ya kuvunja uzio wa shule na kuonya kama wanahisi watoto wanoishi hosteli wataondoka kwa kuchomewa bweni hilo halitawezekana,sababu mabweni yanajengwa kwa manufaa ya watoto wote bila kujali hali ya utajiri na umasikini wa wazazi wao.

“Hatuna mgogoro kati yetu na jamii,kazi yetu ni kuleta maendeleo ya taaluma ya watoto,hatufundishi watoto wa matajiri,tunafundisha watoto wa masikini na wanaovumisha hayo wana ufinyu wa fikra,pia uamuzi wa kujenga hosteli ni wa bodi ya shule si wa mkuu wa shule,”alisema Majaliwa na kueleza hakusomea ukuu wa shule,alisomea ualimu.

Alieleza kuwa shule hiyo ilijengwa mwaka 2003 na Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza, Selemani Khamese wakati yeye (Majaliwa) akifundisha shule nyingine,na baadhi ya wazazi walichnga fedha kumwezesha mmoja wa watuhumiwa kufnya uhalifu wa kuvunja uzio na kuchoma bweni.

Ofisa Elimu Taaluma Manispaa ya Ilemela, Doroth Timoth kwa niaba ya Ofisa Sekondari, Emmanuel Malima, alisema maendeleo ya Kilimani sekondari yana mchango mkubwa wa mkuu wa shule hiyo,aliletwa hapo kusimamia maendeleo miundombinu ya elimu na taaluma na kumtaka mwalimu anyetuhumiwa (si wa shule) apishwe kwenye nyumba ya serikali shule ibaki na amani.

Ofisa wa Polisi,Mkaguzi wa Polisi, Josiah Ndulu kwa niaba ya Mkuu wa Polisi Wilaya ya Ilemela, alisema tukio la kuchoma shule ni kosa la jinai na hakuna msamaha kwa wanaotuhumiwa na kuahidi jeshi la polisi kulishughulikia kuhakikisha wahusika wanakamatwa na kufikishwa mahakamani na kuhusu mgogoro wa ardhi utashughulikiwa na mamlaka husika

Chanzo: www.tanzaniaweb.live