Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Kampuni ya Huduma za Usafirishaji wa Mabasi yaendayo Haraka, maarufu kama Mwendokasi (Udart), Robert Kisena na wenzake, wanaendelea kusota rumande kutokana na upelelezi wa kesi yao kutokukamilika.
Kisena na wenzake wanne, wakabiliwa na mashtaka 19, yakiwemo ya utakatishaji fedha na kuisababishia UDART hasara ya Sh 2bilioni.
Wakili wa Serikali, Elizabeth Mkunde ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam leo Juni 24, 2019, kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
Mkunde ameieleza mahakama hiyo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Augustine Rwizile, wakati shauri hilo lilipofikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa.
"Upelelezi wa kesi hii bado haujakamilika, hivyo tunaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa," amedia wakili Mkunde
Hakimu Rwezile, baada ya kusikiliza maelezo hayo, ameahirisha kesi hiyo hadi Julai 5, 2019 itakapotajwa na washtakiwa wamerudishwa rumande.
Pia Soma
- Mbunge Bwege adai wanyonge hawataichagua CCM 2020
- Profesa Kitila abainisha matatizo ya wahandisi kukwamisha maji vijijini
- Kesi ya Shamimu na mumewe, Mahakama inasubiri ripoti ya Mkemia Mkuu
Katika kesi ya msingi, washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa kati ya Januari Mosi, 2011 na Mei 31,2018 ndani ya jiji la Dar es Salaam, waliongoza genge la uhalifu.
Katika shtaka la pili, linawakabili washitakiwa wanne ambao ni Kisena, Kulwa, Simon na Florence ambalo ni kujenga kituo cha mafuta ya petroli bila kibali kutoka EWURA.
Wanadaiwa kutenda kosa hilo Januari Mosi mwaka 2015 na Desemba 31, 2017 ambapo inadaiwa walijenga kituo hicho eneo la Jangwani bila kibali cha EWURA.
Katika shtaka la tatu washitakiwa hao inadaiwa kwa kipindi hicho wakiwa wakurugenzi walifanya biashara eneo ambalo halijaruhusiwa kujengwa.
Pia katika shitaka la nne inadaiwa waliiba Sh 1.2bilioni mali ya UDART huku mashtaka manne ni utakatishaji wa fedha.
Mengine ni mashtaka manne ya kughushi na kuwasilisha nyaraka za uongo; manne ya wizi; moja kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na moja ni kusababisha hasara UDART.