Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Bosi Takukuru aanza upya majadiliano na DPP

97660 Pic+takukuru Bosi Takukuru aanza upya majadiliano na DPP

Mon, 2 Mar 2020 Chanzo: mwananchi.co.tz

 Dar Es Salaam. Aliyekuwa Mkurugenzi  wa Mipango, Ufuatiliaji na Tathimini wa  Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru),  Kulthum Mansoor ameanza upya mchakato wa majadiliano na Mkurugenzi wa Mashtaka Tanzania ( DPP) ili kuimaliza  kesi hiyo.

Hatua hiyo inatokana na mchakato wa awali kutofikia muafaka.

Mansoor anakabiliwa na mashtaka nane katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu likiwemo la utakatishaji wa Sh1.4bilioni

Mansoor kupitia wakili wake, Elia Mwingira ameleza hayo leo Jumatatu Machi 2, 2020 muda mfupi baada ya kesi inayomkabili mteja wake kuahirishwa.

Akiwa nje ya mahakama, Mwingira aliwaeleza waandishi wa habari kuwa Kulthum ameshaandika barua nyingine ya kukiri na kuomba msamaha kwa DPP ili kesi hiyo iweze kuisha.

"Mteja wangu ameanza upya mchakato wa majadiliano na tayari ameshamuandikia barua nyingine  DPP ya kutaka kumaliza kesi hii,” amesema Mwingira.

Habari zinazohusiana na hii

Advertisement
Amesema hoja hiyo itawasilishwa kesi hiyo itakapotajwa tena mahakamani hapo na Hakimu anayesikiliza,  Godfrey Isaya atakapokuwepo mahakamani.

Hii ni mara ya pili kwa Kulthum kuandika barua, kwani Oktoba 2019 mshtakiwa huyo aliandika barua ya kukiri mashtaka na kuomba msamaha kwa DPP lakini  walishindwa kufikia muafaka.

Januari 6, 2020, wakili Mwingira aliiambia mahakama kuwa waliandika barua ya kukiri na kuomba msamaha kwa DPP lakini walishindwa kufikia makubaliano.

Mwingira amedai kutokana na kushindwa kufikia makubaliano, waliomba upande wa mashtaka kuhakikisha kuwa upelelezi wa kesi hiyo unakamilika kwa wakati.

Leo wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon alieleza Mahakama kuwa kesi hiyo iliitwa kwa ajili ya kutajwa na hakimu anayesikiliza Godfrey Isaya ana udhuru.

Simon amedai mbele ya Hakimu Mkazi, Vicky Mwaikambo kuwa upelelezi wa shauri hilo bado unaendelea, anaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.

Hakimu Mwaikambo  ameahirisha kesi hiyo hadi Machi 16, 2020 itakapotajwa tena.

Mshtakiwa amerudishwa  rumande kutokana shtaka la kutakatisha fedha linalomkabili kutokuwa na dhamana kwa mujibu wa sheria.

Kwa mujibu ya hati ya mashtaka, inadaiwa katika tarehe tofauti kati ya Januari 2013 na Mei 2018, mshtakiwa alighushi barua ya ofa ya Agosti 13,  2003 kwa madhumuni ya kuonyesha kuwa, barua hiyo imetolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo huku akijua kuwa sio kweli.

Katika shtaka la pili, inadaiwa kati ya Januari 2012 na Mei 2017, Upanga Wilaya ya Ilala  mshtakiwa kwa kudanganya alijipatia Sh5.2 milioni   kutoka kwa Alex Mavika ambaye ni mfanyakazi wa Takukuru kama malipo ya kiwanja kilichopo kijiji cha Ukuni Bagamoyo.

Katika mashtaka ya utakatishaji fedha, inadaiwa kati ya Januari mwaka  2013 na Mei 2019 maeneo ya Upanga, mshtakiwa alijipatia Sh1,477,243,000 wakati akijua kuwa fedha hizo ni haramu na ni zao la kosa tangulizi la kughushi.

Chanzo: mwananchi.co.tz