Dar es Salaam. Furaha Masumbuko(14) amesimulia jinsi alivyopigwa na mwajiri wake, Ally Mbela na kupata maumivu sehemu mbalimbali mwilini akidaiwa kuchelewa kurejea nyumbani.
Akizungumza na MCL Digital leo Jumanne Novemba 27, 2018 katika Hospitali ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam alikopelekwa leo akitokea hospitali ya Mtakatifu Joseph, Furaha amesema ana maumivu kwenye mikono, miguu na mbavu.
Binti huyo anayesoma darasa la tatu elimu maalum katika shule ya msingi Mbweni amesema alishushiwa kipigo baada ya kurejea nyumbani saa 12 jioni akitoka shule.
“Kuna mizigo ya mwalimu tuliipeleka nyumbani kwake nikiwa na wenzangu na hivyo kuchelewa kurudi nyumbani. Baba aliporudi saa 2 usiku mama alimueleza na akaanza kunichapa. Maumivu yalipozidi nilikimbilia kwa jirani,” amesema.
Amesema kutokana na maumivu aliyoyapata majirani walimpeleka katika hospitali ya Mtakatifu Joseph alikolazwa kwa siku moja na kuhamishiwa Mwananyamala.
"Mshahara wangu anatumiwa mama, sina baba nataka nikipona nirudi kuendelea na shule,” amesema Furaha ambaye anasomeshwa na mwajiri wake huyo.
Kwa upande wake Mbela amesema alichukua uamuzi huo kutokana na Furaha kuwa na mawasiliano na wanaume.
"Inawezekana kwa bahati mbaya nimezidisha adhabu lakini nilikuwa nafanya hivyo kama mzazi. Nina nia njema naye ndiyo maana nilipomuona ni binti mdogo nikaamua kumuandikisha shule anasoma elimu maalumu,” amesema Mbela.
Hata hivyo, binti huyo alikanusha madai hayo ya kukutwa na barua akidai kuwa ilikuwa ya rafiki yake wa kike.
“Naogopa kupigwa tena ila nataka kusoma nifike walau kidato cha nne. Mama yangu yupo kijijini hawezi kunisomesha, nitarejea kwa walezi wangu. Napenda kusoma,” amesema.
Mjumbe wa shina namba tatu eneo la Boko kati, Magnus Mbebe amesema alipata taarifa za binti huyo kupigwa na alipoamua kwenda katika nyumba hiyo aliamuru apelekwe hospitali.
Mbebe amemtuhumu Ally kuwa licha ya binti huyo kukimbilia kwa jirani, mlezi wake huyo hakumtafuta hadi alipotafutwa na majirani.
"Tunachohitaji mtoto apate matibabu na arudi katika hali yake ya kawaida. Mambo mengine ya kisheria watajua wenyewe sisi jukumu letu ni kuhakikisha usalama wake,” amesema Mbebe aliyekuwa na binti huyo hospitali ya Mwananyamala.