Dar es Salaam. Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam nchini Tanzania linashikilia magari 50 huku 19 yakiwa ya Serikali na 31 binafsi kwa kosa la kupita katika barabara ya mabasi ya mwendo haraka maarufu ‘mwendokasi’
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Oktoba 1, 2019, Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Lazaro Mambosasa amesema kuanzia Septemba 19, 2019 kulifanyika operesheni maalum ya kukamata magari yanayopita kwenye barabara za mwendokasi.
Amesema katika operesheni hiyo, magari 50 yalikamatwa ambapo kati yake magari 19 ni mali ya serikali na magari 31 ni ya watu binafsi.
Kamanda Mambosasa amesema jeshi hilo linatoa onyo kwa madereva wa Serikali na madereva wa magari ya watu binafsi kuacha mara moja kupita kwenye barabara za mwendokasi.
“Jeshi la Polisi linaendelea na operesheni ya kukamata vyombo vyote vya moto na dereva yeyote atakayekamatwa atachukuliwa hatua kali za kisheria, amesema Mambosasa.