Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Bandari bubu nne Tanga zarasimishwa

Sun, 25 Nov 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Tanga. Serikali  imezirasimisha  bandari bubu nne kati ya 48 zilizopo mwambao wa Bahari ya Hindi Mkoa wa Tanga ili kuokoa mapato yaliyokuwa yakipotea.

Akizungumza mara baada ya kutembelea bandari ya Tanga, bandari hizo bubu  leo Ijumaa Novemba 23, 2018, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Atashasta Nditiye amesema mpaka kufikia  Januari 2019, huduma za taasisi za serikali ziwe zimewekwa katika bandari hizo nne.

Amesema lengo la Serikali ni kuziba mianya ya wakwepa kodi, ikiwalenga wanaopitisha bidhaa za magendo katika bandari bubu.

Amesema Tanzania kuna bandari bubu zaidi ya 300, hivyo Serikali ina mkakati wa kufanya msako maalum wa kuhakikisha bandari zote bubu zinakufa ili mapato ya Serikali yaongezeke pamoja na mapato ya mtu mmoja mmoja.

"Ifikapo mwishoni mwa Januari nataka kuona mnaweka ofisi za Serikali katika maeneo yaliyorasimishwa ili tuweze kukusanya kodi ya Serikali,” amesema Nditiye.

Naibu Waziri huyo pia ametumia fursa hiyo kuwataka wananchi na wafanyabiashara  wanaoendelea  kutumia bandari  bubu  hizo waache mara moja  kwani hazitambuliki.

Kwa  upande wake, meneja wa bandari Mkoani Tanga, Parcival Salama  amesema kwa  mkoa wa Tanga ni bandari mbili tu ambazo zinatambulika  kisheria ambazo ni bandari ya Tanga na  bandari  ya Pangani.

Salama  amezitaja  bandari bubu ambazo  zimerasimishwa  rasmi ni  Kipumbwi, Kigombe, Mkwaja  zilizopo Pangani na Moa  wilayani Mkinga.

Meneja  huyo amesema mkoa  wa Tanga kuna bandari bubu 48 nakwamba  kwa upande wa Mkinga  ziko 12 , Tanga Jiji 20, Muheza moja pamoja na wilaya ya Pangani ziko 15.

Mapendekezo ya kurasimisha bandari hizo bubu yametokana na utafiti uliofanywa na menejimenti ya bandari ya Tanga kutokana na maelekezo yaliyotolewa na serikali.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Moa, Rambazo  Mohamedi amesema wamefurahishwa na uamuzi wa serikali wa kuamua  kuzirasimisha  bandari  hizo na wako tayari  kutoa  maeneo kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za serikali.



Chanzo: mwananchi.co.tz