Mbeya. Polisi mkoa wa Mbeya linamshikilia baba mzazi wa marehemu Rose Japhet (6), mkazi wa Msewe kata ya Igurusi-Mbarali, mkoani humo na mfanyabiashara mmoja kwa tuhuma za kuhusika kwa mauaji ya mtoto huyo ili kujipatia utajiri.
Taarifa iliyotolewa jana Jumamosi Mei 11 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ulrich Matei ilisema watu wanaotuhumiwa kuhusika na mauaji ya mtoto huyo ni baba mzazi wa mtoto huyo na mfanyabiashara anayemiliki shule ya sekondari wilaya ya Mbeya.
Kamanda Matei alisema Mei 3 muda wa saa 3:00 usiku katika eneo la msitu wa Hifadhi wa Chimala-Mbarali, mtoto huyo alikutwa ameuawa kwa kunyongwa shingo kisha kukatwa kanyagio la mguu wake.
Alisema katika msako wa polisi, kanyagio la mtoto huyo lilikutwa limefukiwa eneo la Mbalizi wilaya ya Mbeya.
"Chanzo cha tukio hili ni tamaa ya kupata utajiri. Baba mzazi wa marehemu mtoto huyo alimtoa mwanae huyo kwa mfanyabiashara huyo (mtuhumiwa wa pili) ambaye ni mmiliki wa shule ya sekondari kwa malipo ya Sh5 milioni,” alisema.
Lengo auawe na kisha kanyagio la mguu wa kulia na kupatiwa mfanyabiashara huyo na apeleke kwa mganga ili amtengenezee dawa ya utajiri aweze kufanikiwa kwenye biashaara zake za shule anayomiliki," alisema Kamanda Matei.
Habari zinazohusiana na hii
- Baba mzazi adaiwa kuua mwanaye kwa malipo ya Sh5 milioni
- Wajane wajitokeza kugombea nafasi walizotamani waume zao kabla ya kuuawa