Dar es Salaam. Mahakama ya Wilaya ya Temeke imemsomea maelezo ya awali mshtakiwa Haruna Abdu (54) mkazi wa Mbagala Mwanamtoti kwa tuhuma za kumbaka na kumlawiti binti yake wa kumzaa (12).
Akisoma maelezo hayo mwendesha mashataka, Salome Assey alisema kuanzia Januari mwaka 2017 hadi Februari 2019 mshtakiwa alikuwa akimbaka mwanaye wa kumzaa na kumuingilia kinyume na maumbile.
Amesema ilipofika Februari 2019, mtoto huyo alishindwa kwenda shule kutokana na vitendo alivyofanyiwa na mzazi wake huyo.
Alisema alipohojiwa na mwalimu wake aliyefahamika kwa jina la Ngulula, mtoto huyo alimueleza kuwa alikuwa anafanyiwa vitendo hivyo na baba yake ndipo taarifa ilipotolewa kituo cha polisi.
Ameongeza kuwa baada ya hapo, mtoto huyo alipewa fomu namba 3 ya Polisi (PF3) kwa ajili ya uchunguzi wa hospitali na baada ya hapo uliandaliwa mtego kwa ajili ya kumkamata mshtakiwa.
Aliongeza kuwa Machi 4, 2019 wakati mshtakiwa anarudi nyumbani akitokea kazini alikamatwa na polisi akiwa anataka kumbaka bintiye.
Pia Soma
- Mfumko wa bei wapanda Mei
- Kazakhstan yapata rais mpya
- Rais Magufuli awaapisha Waziri Bashungwa, Kichere na Mhede
Alisema baada ya hapo mshtakiwa alipelekwa kituo cha Polisi Mbagala kwa hatua za kisheria.
Abdu amesomewa shtaka la kulawiti na kumbaka mwanaye wa kumzaa lenye jalada namba CC233/2019 mbele ya Hakimu Mkazi Mariam Mfanga.
Hata hivyo, mshtakiwa alikana shitaka hilo na kuiambia mahakama kuwa hakutenda kosa hilo na kesi hiyo itasikilizwa tena Juni 24 mwaka huu ambapo mashahidi sita akiwemo binti mwenyewe watapeleka vielelezo.