Raia mmoja wa Misri ambaye alikuwa ameenda kudai deni lake kutoka kwa jirani yake amefariki dunia baada ya kudungwa kisu mara nane katika mapigano kwenye mtaa wa Jamhuri jijini Nairobi.
Marehemu aliyetambulika kama Ayman Alsaid inasemekana alidungwa kisu mara nane na mshukiwa aliyejaribu pia kujiua.
Polisi walioitwa na jirani baada ya kusikia vurugu katika ghorofa ya Orange mtaani Jamhuri walikuta watu watatu wakiwa na majeraha ya kudungwa kisu.
Polisi walisema Alsaid na mwenzake alienda kwa nyumba ya mshukiwa na kutaka walipwe deni lao walilokuwa wakimdai. Mdaiwa huyo alikasirika na kwenda jikoni, akachukua kisu na kumchoma mdai wake mara nane huku mwenzake akichomwa kisu kwenye paja kabla ya kujigeuzia kisu hicho mwenyewe na kujikata koromeo.
Watatu hao walikimbizwa katika hospitali ya Coptic ambapo Alsaid alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu.