Mkazi mmoja wa kijiji cha Manyire wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha, Adael Willbad (21) anatuhumiwa kumuua kaka yake kwa kisu na kumjeruhi mama yake mzazi, Editha Vavoiyo katika ugomvi wa kugombea jiko la kupikia.
Tukio hilo limetokea usiku wa Mei 7, 2022 nyumbani kwa familia hiyo mara baada ya kuzuka mzozo baina ya marehemu aliyejulikana kwa jina la Ezekiel Willbard (24) na mdogo wake jambo lililomlazimu mama yao kuingilia kati.
Mwili wa marehemu umehifadhiwa hospitali ya Nkoranga kwa uchunguzi zaidi huku mama yao akilazwa hospitalini hapo kwa matibabu.
Akizungumza leo Mei 8, 2022, Mwenyekiti wa kijiji cha Manyire, Evarest Mallya amesema chanzo cha mzozo huo ulitokana na wanandugu hao kugombea sehemu ya kupikia ambapo mama yao mzazi aliwakataza na kuwaambia wakatafute sehemu nyingine kwani jiko hilo ni mali yake.
“Baada ya kuona mzozo unazidi kuwa mkubwa mama yao alichukua uamuzi wa kumwaga maji katika jiko hilo ili wote wakose, "amesema.
Hata hivyo kitendo hicho kilimkera mtuhumiwa ambaye alichukua kisu na kumjeruhi mama yake tumboni ambaye alianguka chini na kaka yake alipoenda kusaidia alimchoma na kisu na kufariki papo hapo.
Aidha, Mwenyekiti amesema mtuhumiwa huyo alijaribu kutoroka lakini wananchi walifanikiwa kumkamata katika eneo la Gomba alikokuwa amekimbilia kujificha.
Kamanda wa polisi Mkoani hapa, Justine Masejo hakuweza kupatikana kuzungumzia tukio hilo licha ya simu yake ya mkononi kuita kwa muda mrefu bila kupokelewa.