MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam imemhukumu mkazi wa Kivule jijini humo, Cosmas Chacha kifungo cha miaka 15 jela na kulipa faini ya Sh milioni 3 baada kumtia hatiani kwa makosa matatu ya kuwakeketa wanawe watatu wenye umri chini ya miaka 18.
Hakimu Mkazi Mkuu Rashid Chaungu alitoa hukumu hiyo jana baada ya Mahakama kuthibitisha mashitaka yote pasipo kuacha shaka yoyote.
Hakimu Chaungu alisema Chacha atatumikia miaka mitano jela kwa kila kosa na adhabu hiyo itakwenda pamoja.
Alisema pia mshitakiwa huyo atatakiwa kulipa faini ya jumla ya Sh milioni 3 sawa na Sh milioni moja kwa kila mtoto.
Kabla ya kusomwa hukumu hiyo Wakili wa Serikali Esther Martin aliyekuwa akiwakilisha jamhuri aliomba Mahakama itoe adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine.
Ilidaiwa mahakamani kuwa, Desemba 8, 2019 katika eneo la Kivule jijini Dar es Salaam Chacha alitenda kosa la kuwakeketa watoto wake wa kuwazaa jambo ambalo ni kinyume cha sheria.