Askari wa vikosi vya Ulinzi na Usalama vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Juma Abdalla Khamis (34) amekamatwa na kete 3198 zinazodhaniwa kuwa ni heroin.
Akizungumza nasi kwa njia ya simu jana Jumamosi Aprili 15, 2023, kamishna mkuu wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar, Kanali Burhan Zubei Nassor amethibitisha kukamatwa askari huyo Aprili 11, 2023 katika uwanja wa ndege wa Pemba.
Kwa mujibu wa kamishna Burhan, bila kutaja askari huyo ni mtumishi wa kikosi gani kwa kile alichoeleza kutoharibu upelelezi, amesema alikamatwa na maofisa wa mamlaka hiyo saa 10 jioni katika uwanja wa ndege Pemba.
“Mtuhumiwa ni mkazi wa Kibanda Maiti Unguja, hizi ni taarifa za awali bado uchunguzi unaendelea taarifa zaidi zitatolewa baada ya uchunguzi kukamilika,” amesema.
Kamishna huyo amesema wataendelea kushirikiana na mamlaka zote zinazohusika kudhibiti vitendo hivyo.
Septemba mwaka 2022, Athumani Akida Juma (32) mkazi wa Nungwi alikamatwa na pakiti 20 zenye kete 2,401 zinazodaiwa ni heroin.
Pia, Februari mwaka huohuo Jeshi la polisi liliwakatama wanawake wawili wakiwa na heroin zenye uzito wa kilo 5.62 katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Abeid Aman Karume.