ASKARI wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi la Tanzania (JWTZ), Jacob Sylvester na mwenzake wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya mauaji ya Abdul Ahmad ‘Bosnia’.
Mbali na Sylvester, mshitakiwa mwingine ni mfagiaji wa Suma JKT na mkazi wa Buza, Almas Selemani.
Akisoma mashitaka hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Yusto Ruboroga, Wakili wa Serikali, Neema Mushi alidai washitakiwa walitenda kosa hilo Novemba 15, 2020.
Alidai washitakiwa hao kwa makusudi walimuua Abdul Ahmed kinyume cha sheria. Upande wa mashitaka ulidai upelelezi wa kesi hiyo haujakamlika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.
Hakimu Ruboroga aliahirisha kesi hiyo hadi Machi 16, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa. Bosnia alikuwa Mshauri wa Klabu ya African Sports ya jijini Tanga iliyoko Daraja la Kwanza.