Shinyanga. Jeshi la polisi mkoani Shinyanga linamsaka Suzana Richard mkazi wa Uzogole Manispaa ya Shinyanga kwa tuhuma za kumjeruhi mume wake kwa kuchoma kisu ubavuni baada ya kutokea kutoelewana kati yao.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Debora Magiligimba amesema mtuhumiwa huyo anadaiwa kumchoma kisu mumewe Mpemba Gamba (48) katika tukio lililotokea saa 6:00 usiku wa Aprili 11, 2020 wakiwa nyumbani kwao mtaa wa Uzogole Manispaa ya Shinyanga.
Kabla ya tukio hilo, wanandoa hao wanadaiwa kuwa na mvutano kuhusu kurudiana baada ya kutengana siku tatu zilizopita.
"Mtuhumiwa alikimbia na kutokomea kusikojulikana. Polisi tunaendelea kumsaka ili kumfikisha mahakamani kujibu tuhuma dhidi yake," amesema Kamanda Magiligimba
Akifafanua, Kamanda Magiligimba amesema mtuhumiwa na mume wake walitenga siku tatu kabla ya tukio na siku hiyo alirejea nyumbani kumshawishi mume wake warudiane na baada ya ombi lake kukataliwa ndipo alimjeruhi mwenzake kwa kumchoma kisu ubavuni.
"Tunawasisitiza wanandoa na watu walioko kwenye mahusiano ya mapenzi kuepuka kujichukulia sheria mkononi wanapotofautina badala yake watafute msaada wa kisheria au ushauri wa wazazi, wazee na viongozi wa kijamii na kidini," ameshauri Kamanda Magiligimba.