Dar es Salaam. Meneja wa tawi la kampuni ya Neelkani Salt Limited, Mohammed Alikhan amefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi.
Katika Kesi hiyo namba 114 ya mwaka 2019, Alikhan anakabiliwa na mashtaka mawili ya utakatishaji fedha na wizi wa katoni 45,919 za chumvi zenye thamani ya Sh413.5 milioni.
Akimsomea mashtaka leo Jumanne Oktoba 22, 2019 wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Janeth Mtega amesema Alikhan alitenda makosa hayo kati ya Januari Mosi,2018 na Julai 29, 2019.
Wakili Simon amedai kati ya siku hizo mtaa wa Arusha Ilala, Alikhan akiwa meneja wa tawi la kampuni hiyo aliiba katoni hizo za chumvi aina ya Neel mali ya mwajiri wake zenye thamani ya Sh412.8 milioni.
Amedai mshtakiwa huyo pia katika kipindi hicho aliiba chumvi aina ya Neel Gold zenye thamani ya Sh720,000.
Wakili Simon amedai katika kipindi hicho mshtakiwa alitakatisha Sh 413.5 milioni wakati akijiua fedha hizo zimetokana na zao la makosa la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na wizi akiwa mwajiliwa.
Pia Soma
- Shahidi aeleza alivyopata taarifa za mkutano wa Zitto
- Maombi ya wadau kwa Serikali ya Tanzania kuhusu ubunifu haya hapa
- Lukuvi apiga marufuku maofisa ardhi kutoa ofa za viwanja
Baada ya kusomewa mashtaka hayo hakuruhusiwa kuzungumza chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi.
Upande wa mashtaka umedai upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na mshtakiwa kupelekwa rumande. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Novemba 5, 2019.