Dar es Salaam. Thomas Mgoli(37), mkazi wa Buguruni amefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashtaka matatu, likiwemo la kujifanya ofisa wa Idara ya Usalama wa Taifa.
Imedaiwa mahakamani hapo kuwa lengo lake ilikuwa kumsaidia aliyekuwa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi kupata dhamana.
Alipandishwa mahakamani hapo jana Ijumaa Septemba 20, 2019 na kusomewa mashtaka matatu ya kujifanya ofisa wa idara hiyo, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kutakatisha fedha.
Mbele ya Hakimu Mkazi mfawidhi, Kelvin Mhina wakili mkuu wa Serikali, Faraja Nchimbi amedai mshatakiwa anakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi.
Nchimbi amedai kati ya Desemba Mosi, 2017 na Agosti 2019 maeneo ya mahabusu ya Keko, mtuhumiwa alijifanya mtumishi wa umma aliyeajiriwa na Idara hiyo huku akijua kuwa si kweli.
Katika shtaka la pili kati ya Agosti 17 na Agosti 29, 2019 jijini Dar es Salaam akiwa na nia ya kulaghai alijipatia Sh280,500 kutoka kwa Lucy Ngongoseki kupitia simu ya mkononi akidai atamsaidia Malinzi kupata dhamana.
Pia Soma
- RC mpya Morogoro ateuliwa akiwa barabarani kwenda Dodoma
- Kocha Spurs aanza visingizio mapema
- Neville aibeba Chelsea, aiponda Liverpool
Mshtakiwa hakutakiwa kujibu chochote kutokana na kesi inayomkabili mahakama hiyo kutokuwa na mamlaka ya kutoa dhamana.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Oktoba 4, 2019.